Home » 2017 » December » 1 » Alibaba na wezi 40 Part 11
17:53
Alibaba na wezi 40 Part 11

SEHEMU YA KUMI NA MOJA

WEZI THELATHINI NA TISA

Kutoka sehemu ya kumi:

Baada ya mpango wa mwizi wa pili kufeli, sasa kiongozi wa wezi akaamua kutumia mbinu zake mwenyewe kwenda kuitafuta nyumba ya Kassim, na hatimaye akaipata. Sasa kiongozi wa wezi akapanga mpango wa kwenda kwa Alibaba.....

Endelea sehemu ya Kumi na moja.

Wezi walipofika mjini wakaanza kazi ya kutafuta punda kama walivyoagizwa na kiongozi wao.

“Ishirini? Unahitaji punda ishirini?” aliuliza mtu mmoja kwa mshangao.

“Ndio, hivyo ndivyo nilivyosema, ishirini,” mwizi  alijibu.

“vizuri, sina punda ishirini,” alijibu yule mtu, “lakini nitakuuzia wawili. Wako kwenye uwanja wangu, nyumba ya nyumba. Njoo nikuoneshe.”

Wezi walikuwa wakifuata mpango mzima wa kiongozi wao. Kwanza, walizunguka mji mzima kutafuta wenye punda. Wenye punda walipooneshwa sarafu za dhahabu kwenye mikono ya wezi wale, wengi wao walifurahi sana na kutaka kuwauzia.

Mwisho wa wiki ile, wezi wote walinunua punda wote ishirini kama walivyoagizwa na kiongozi wao. Punda wakubwa, punda wadogo na waliozeeka, wenye rangi ya kijivu, weusi na weupe.

“Hivi kwanini kiongozi wetu anataka punda hawa?” mwizi mmoja alimuuliza mwenzie. “amechanganyikiwa nini?”

“Mh! Sijui..”  mwizi wa pili alijibu. “sisi tufanye tu kama alivyotuagiza.

Wakati wezi wakiwa mjini wakinunua punda, kiongozi wao alikuwa akitembelea kwa watengeneza vyungu na mitungi nje ya mji kidogo. Fundi mmoja alikuwa akipaka rangi katika mtungi mmoja mkubwa  uliotengenezwa kwa udongo wa mfinyanzi.

“Unahitaji mtungi, rafiki yangu?” aliuliza mtengeneza mitungi.

“Ndiyo nahitaji.” Alijibu kiongozi wa wezi. “lakini nahitaji unitengenezee mitungi mikubwa arobaini ya kuwekea mafuta. Yote lazima iwe na mifuniko, lakini mifuniko hiyo isiwe yenye kukaza sana wakati wa kufunika mitungi. Mitungi lazima iwe imekamilika ifikapo mwisho wa wiki hii. Ni muhimu sana!”

Mtengeneza mitungi akamuangalia sana kiongozi wa wale wezi. “Wiki moja haitoshi kutengeneza mitungi yote arobaini.” Alimjibu. “Sina uhakika kama naweza kuifanya kazi hii.”

“ukiweza, nitakulipa mfuko mzima wa dhahabu,” alisema yule kiongozi wa wezi. Akanyanyua lile fuko la dhahabu juu kisha akanyanyua upanga wake mkali juu. “lakini usipoifanya kazi hii, unajua mwenyewe kitakachotokea.”

Mtengeneza mitungi akatikisa kichwa kwa ishara ya kukubali na haraka sana akaanza kuifanya ile kazi ya kutengeneza mitungi arobaini.

“nitamuomba kaka yangu anisaidie,” mtengeneza mitungi alijisemea moyoni. “ na shemeji yangu pia atanisaidia. Kama tukifanya kazi hii kwa juhudi, natumaini tutaimaliza ndani ya huu muda wa wiki moja.”

Baada ya wiki moja mitungi ile ilikuwa tayari, kiongozi wa wezi akaenda kwa muuza mafuta mkubwa sokoni na kujaza mtungi mmoja mafuta. Kisha akamtuma mmoja wa wezi akawalete wale punda ishirini aliowanunua.

Kiongozi wa wezi akapakia kwa kila punda mitungi miwili miwili. Kisha akawapeleka mpaka kule msituni kukutana na wezi wengine waliobakia huko.

“Sasa ni sehemu ya pili ya mpango wangu,” alisema kiongozi wa wezi. “Kila mmoja wenu aingie ndani ya mtungi mmoja.”

“Tuingie kwenye mitungi? Kwanini?” aliuliza mmoja wa wezi . “Na tutapumuaje?”

“mifuniko yake haikazi sana.” Alijibu kiongozi wa wezi. “Msihofu – mtaweza kupumua. Chukueni panga zenu na ngao muingie nazo ndani ya mitungi kwasababu zina kazi yake maalumu huko. Tutaenda kwenye ile nyumba mkiwa nyote thelathini na tisa ndani ya mitungi thelathini na tisa.”

“Na vipi kuhusu huo mtungi wa arobaini? Utaingia wewe?” mmoja aliuliza.

“Hapana!” alijibu kiongozi wao. “Nitavaa mavazi ya kuficha uso na nitawaongoza punda wote mpaka huko. Huu mtungi wa arobaini umejaa mafuta – ni moja ya mpango wangu, nitajifanya ni muuza mafuta. Nitawaongoza punda wote mpaka kwenye nyumba ambayo Mustafa alinionesha. Nitawaomba watu wa nyumba ile kama watanipa msaada wa kulala usiku mmoja kwasababu niko kwenye safari ndefu na ninapoelekea ni mbali sana. Kisha akiniruhusu tu na kunipa nafasi ya kuwaingiza punda hawa ndani, sasa itakuwa ni nafasi yenu nzuri ya kujitokeza na kumaliza kazi. Hapo atajuta kutuibia mali zetu.”

Baada ya kusema hayo kila mwizi alichukua upanga na kuingia ndani ya ile mitungi.

Kiongozi akavaa mavazi ambayo uso wake hauwezi kuonekana vizuri, kisha akaanza safari ya kuelekea mjini na punda ishirini waliobeba mitungi arobaini.

Muda ambao alikuwa ameshafika mjini, tayari giza lilikua limeshaanza kutanda.

 

Muda mfupi tu akafika katika nyumba ile yenye maua mazuri na paka wa rangi ya machungwa. Kulikuwa na mtu aliyekaa kwenye stuli nje ya nyumba hiyo. Alikuwa akitazama watu wanaopita njia na akisikiliza sauti za ndege mbalimbali wakiwa wanatoa sauti za kujibembeleza kwaajili ya kulala.

Kiongozi wa wezi alipomuona yule mtu nje, alisimamisha punda wake wote.

“Habari ya saa hizi.” Kiongozi alimsalimia Alibaba.

“Nzuri,” alijibu Alibaba kwa hali ya kushangaa na kusimama kwa kuheshimu mgeni. “Naitwa Alibaba. Naweza kukusaidia nini rafiki yangu?”

“Mimi ni muuza mafuta, natokea mbali sana.” Alijibu yule kiongozi wa wezi. “Punda wangu wamechoka sana na hata mimi vilevile. Tunaweza kukaa kwako usiku huu tu kisha kesho asubuhi tutaondoka. Hatutakuwa na usumbufu wowote tafadhali.”

“Umesema wewe ni muuza mafuta. Mafuta hayo yako wapi?” aliuliza Alibaba kutaka kuhakikisha kwamba yule mtu ni mkweli.”

Yule kiongozi wa wezi akamuoneshea kwenye ule mtungi ambao alijaza mafuta. “Yapo kwenye mitungi hii, ni mafuta bora na mazuri sana kuliko ya aina yoyote ile. Ungependa kuyaona?”

Akafungua mfuniko wa ule mtungi wenye mafuta na Alibaba akachungulia ndani yake. Kisha akanyanyua macho kumtazama kiongozi na kutabasamu.

“Karibu sana ndani ukae,” alisema Alibaba. “ Walete punda wako uwani huku.”

“Ahsante sana. Una roho nzuri sana,” alisema kiongozi wa wezi. Kisha akawaongoza punda wale mpaka ndani.

“Naona pia punda hawa wanahitaji chakula na kupumzika,” Alibaba alimwambia kiongozi wa wezi. “Watue hiyo mizigo yao chini na wapeleke kwenye zizi. Wape nyasi huko na maji ya kutosha.”

Hivyo kiongozi wa wezi akashusha ile mitungi na kuwapeleka punda kwenye zizi. Akaiacha ile mitungi arobaini kwenye uwanja wa ndani wa nyumba ikiwa imepangika kwa mstari mmoja.

“Unaweza tu ukaiacha mitungi hii hapo uwanjani haina neno kwa usiku mmoja,” alisema Alibaba. “Twende ndani nikakupatie chochote ule ili upumzike.”

Akamkaribisha yule kiongozi wa wezi ndani na kumuita Marjane mtumishi wake.

“Mke wangu yuko wapi?” Alibaba alimuuliza Marjane.

“Wameenda kulala. Wote na mwanao pia leo wameingia ndani kulala mapema sana.” Alijibu Marjane.

“Sawa basi, Marjane. Mtengenezee chakula huyu mtu, tafadhali.” Alisema Alibaba.  “Ni mgeni wetu na ni vema tukamkirimu.”

Marjane akavuta pumzi za kuonekana kuchoka. Alikuwa ameshachoka na kazi za siku ile na alikuwa anajiandaa kwenda kulala.

“Sawa bosi,” Alijibu Marjane na kuelekea jikoni. Muda mfupi tu chakula kilikuwa tayari.

Kiongozi wa wezi alikula vizuri sana usiku ule, Marjane alimuandalia wali wa njegere na nyama na alifaidi sana chakula kile.

“Mpango wangu unaenda vizuri sana.” Alijisemea moyoni. “Muda si mrefu Alibaba atakuwa mtuhumiwa wangu.”

Alibaba akaingia jikoni wakati Marjane akiosha vyombo vilivyotumika usiku ule.

“Naenda kulala sasa,” alimwambia. “Marjane, tafadhali hakikisha mgeni wetu anapata kila kinachohitajika. Asubuhi nitenda mapema sana kuoga hivyo nitahitaji sabuni na taulo.”

Hivyo Marjane akaenda kumchukulia sabuni na taulo na Alibaba akaenda kulala. Kiongozi wa wezi akamwambia Marjane kwamba angependakupata hewa safi ya nje kidogo kabla ya kwenda kulala.

Endelea sehemu ya kumi na mbili ya hadithi hii…………….

 

Category: Stories & Entertainment | Views: 846 | Added by: badshah | Rating: 0.0/0
Total comments: 1
1 zakwan  
0 Spam
Best story

Name *:
Email *:
Code *: