Home » 2017 » October » 26 » Alibaba na wezi 40 Part 7
18:27
Alibaba na wezi 40 Part 7

SEHEMU YA SABA

DHAHABU ZAIDI KWA MUSTAFA

Kutoka sehemu ya sita:

Kwa siri kabisa, Alibaba na familia yake pamoja na mke wa Kassim na mfanya kazi wao Marjane walijitahidi kufanya siri kubwa sana juu ya kifo cha Kassim. Walifanya kila aina ya utaratibu wa mazishi na kuweza kufanikiwa kumzika Kassim.

ENDELEA SEHEMU YA SABA

Kule msituni nako, wale wezi 40 walikuwa wakiendelea kupeleka dhahabu zao kwenye pango kama ilivyo kawaida yao, siku hiyo walikuwa katika hali ya furaha. “Hebu tukifika tuangalieni kama dhahabu zetu zote zipo!” alisema yule kiongozi wao, “hakuna mtu atakayethubutu kutuibia tena. Ile maiti tulioining’iniza mtu yeyote atakayeingia na kuiona ataogopa sana na ndio itakuwa fundisho!”

Wale wezi walicheka kwa furaha huku wakiwa njiani na farasi wao wakielekea pangoni. Walipofika kwenye lango la pango lile la ajabu wakashuka kwenye farasi wao wote na kusimama mbele ya lile lango la mwamba. “Fungukaaaaa sesmiiii!!!” alisema yule kiongozi wao. Lango likafunguka, na yule kiongozi wao akaingia ndani kidogo huku akitazama kona zote za lile pango.

“Umepotea!!!, mwili umepoteaaa!!!” alisema kiongozi wao huku akipiga mguu chini kwa hasira, kisha akawageukia wale wezi wenzake na kuwatazama. “Niliwaambieni tu!! Hapa kuna mwizi mwengine!!” alisema kwa hasira, “tumemuua mmoja, lakini mwenzake aliporudi alikuja kuuchukua mwili wa mwenzie”.

Yule kiongozi wao alipoendelea kuangalia pangoni, akaona kitu ambacho ndio kilizidi kumpatia hasira, aliona dhahabu nyingi zimepotea zaidi ya mara ya kwanza.

“Lazima tutafute na tumjue huyu mtu mwingine ni nani na tujue anaishi wapi” alisema huku wakiingia ndani ya pango, “na tukimpata lazima na yeye tumuue”

“Lakini tutamjuaje huyu mtu?” mmoja wa wale wezi aliuliza.

“kwa sababu ameichukua maiti ya mwenzie, lazima mmoja wetu aende mjini” alisema kiongozi wao, “akifika mjini ajaribu kusikiliza fununu za watu wakiongelea habari ya msiba au kupotea kwa mtu. Tukishajua mahala ambapo pana msiba au mahali ambapo huyo mtu ametangazwa kupotea, itakua rahisi kumpata huyo mwingine”

“Nitakwenda!” mmoja wao alisema, “nitatafuta mpaka nimjue huyo mtu ni nani na mahali anapoishi.”

“Una akili sana! Na ni mjanja” alijibu kiongozi wao, “hii ni kazi muhimu sana!”

“Nina uhakika nitampata huyo mtu!” alisema yule mwizi.

“Hivyo jitahidi uende!” alisema kiongozi wao. “lakini lazima ubadilishe sura yako kwa kuziba na nguo mdomoni na pia vaa kanzu ndevu kisha ujifanye wewe ni msafiri tu. Waambie watu kwamba wewe ni mgeni hapo mjini. Chukua dhahabu kidogo kwaajili ya kuwashawishi watu wakupe taarifa unayotaka, ongea nao vizuri na uskilize kwa makini sana wanachokisema.”

Baada ya kusema hayo wakatoka nje ya pango kisha yule kiongozi akasema neno la siri “fungaaaa sesmiii!!”. Kisha lile lango likajifunga kwa nguvu.

Siku iliyofuata, yule mwizi akavaa kama alivyoagizwa. Alivaa kanzu ndefu na koti kubwa lenye kofia kama jaketi la mvua. Akaanza safari ya mjini mpaka sokoni, akaongea na wafanyabiashara mbalimbali hapo sokoni. Akapata taarifa nzuri tu kuhusu mauzo ya kamba, nyama, kuku na vinginevyo pale sokoni, kisha akenda kwenye mgahawa nakuulizia bei ya mkate, kisha akaenda kwenye bustani mbalimbali za pale mjini. Alizungumza na matajiri na pia alizungumza na masikini, alizungumza na mamia ya watu pale mjini lakini hakuweza kupata taarifa yoyote pale mjini. Hakuna mtu yeyote aliyezungumza kuhusu mauaji, wala hakuna yeyote aliyezungumza kuhusu hazina za pangoni.

“Nimezungumza na mamia ya watu lakini hakuna hata mmoja aliyenipa taarifa ya kile ninachokitafuta.” Yule mwizi alijisemea mwenyewe. “hakuna hata mtu aliyezunguzia juu ya mtu aliyekufa. Bora tu nirudi kwa kiongozi wangu nimwambie kwamba nimeshindwa. Lakini atakuwa na hasira sana.”

Yule mwizi alizunguka mchana kutwa mpaka akachoka. Akaamua kukaa chini karibu na kibanda cha fundi nguo na kuangalia viatu vyake na akaona vimetoboka chini kwa shida ya safari ya mchana kutwa.

Alivivua viatu vile. Kulikuwa na mzee mmoja ndani ya kibanda kile cha fundi nguo, yule mwizi akavipeleka kule ndani.

“Angalia matundu haya kwenye viatu vyangu” mwizi alimwambia yule mzee huku akimuonesha. “Sasa hivi jua litazama, lakini naona kama macho yako hayaoni vizuri mzee, hivi unaona kweli?”

“Ooh!ndio naona matundu haya” alisema Mustafa (fundi nguo). “Macho yangu mazuri tu, mimi ndio fundi nguo maarufu hapa mjini, naona vizuri kiasi cha kuweza kuweka uzi kwenye sindano na kushona. Hakuna mtu hapa mjini anayeweza kushona vizuri kunishinda.” Aliendelea kusema. “Na ukizingatia siku chache zilizopita nilikuwa na kazi ngumu sana, nilishona suti ya maiti mmoja katika ghala lenye giza. Ilikuwa ni msichana mmoja wa kazi alikuja na kunipeleka nyumbani kwao kwaajili ya kazi hiyo. Hivyo alinichukua mpaka kwake.”

“Maiti!!?” yule mwizi alisema kwa mshangao fulani.

Endelea sehemu ya nane ya hadithi hii…………….

 

Category: Stories & Entertainment | Views: 644 | Added by: badshah | Rating: 1.0/1
Total comments: 1
1 zakwan  
0 Spam
Mr Admin we want part8please

Name *:
Email *:
Code *: